Skip to main content

NAMNA MATUNDA YANAVYOPEWA THAMANI NA WENZETU

Papai na Parachichi-2-pic by F Macha

Imekuwa kazi sana kupiga picha ya mseto huu mzuri na mtamu leo kabla ya kuushughulikia.
Afrika imejaaliwa mimea, madini, rutuba na hali ya hewa safi.
Takribani vyakula vyote tunavyohitaji wanadamu hupatikana bara hili. Lakini pamoja na hayo uhai wetu mfupi kuzidi wengine duniani. Kufuatana na orodha ya wastani wa maisha iliyotolewa na shirika la Ujasusi Marekani (CIA)na Umoja wa Mataifa mwaka 2011- nchi zinazoongoza kwa maisha marefu ni Japani na chini kabisa ni Afrika.
Machenza na Nanasi
Wajapani wanaishi hadi miaka 90 kuendelea , Ulaya, Marekani na China kati ya 75 hadi 90; nchi za bara Asia (mathalan India) miaka 65 kuendelea; mwisho ni Afrika yenye taifa la Angola mkiani (miaka 40). Tanzania imewekwa na wastani wa miaka 50 hadi 53.
Kombu la Kijapani
Msingi wa sababu zinazowafanya watu wasiishi muda mrefu ni maendeleo ya uchumi-jamii na siasa.
Lakini kiini cha wewe kuishi (mbali na elimu, makazi bora na furaha moyoni )ni CHAKULA BORA NA NAMNA UNAVYOKILA.

Wajapani mathalan wanasifika kwa kula vyema- hawali misosi mikubwa mikubwa kama sisi. Ulaji wao ni mdogo mdogo, wa mara kwa mara- hawajazi sana matumbo. Halafu kuna vitu wanavyokula ambavyo husaidia sana kukarabati na kuhifadhi mwili. Mfano mzuri ni mimea ya baharini. Kuna mmea uitwao Kombu ambao unauchemsha na kuyatumia maji yake kwa kupikia mchuzi, chai, nk. Moja ya faida ya “Kombu” ni kukinga na kuuponyesha mwili kutokana na maradhi; pili, kuongeza nguvu za nywele, ngozi na maisha kijumla. Ndiyo maana nadra sana kumwona Mjapani asiyekua na nywele nyingi, hata akiwa mzee- huwaoni wana mvi. Mvi ni dalili ya ukosefu wa madini mwilini.
Wana afya.
Pumpkin Seeds
Mbegu mbichi kama hizi za Maboga zina faida kubwa sana mwilini : mafuta asilia yasiyodhuru moyo-kama nyama, kinga maradhi, ujenzi na kukarabati ngozi, mifupa, kucha, nywele, kuupa mwili nguvu za rijali nk.
Wenzetu nchi zilizoendelea wanathamini sana matunda na mboga mboga. Si ajabu leo wanaishi maisha marefu kutuzidi.
Sisi tumevijaza vyote hivi, TELE, lakini hatuvithamini.
Zamani nikiwa mtoto ilikuwa kawaida mapishi kuwa na mboga za majani na saladi (kachumbari) leo kutokana na kuingizwa kwa utamaduni wa “vyakula vya haraka “ (“junk”) na “ladha” –vyenye CHUMVI NA MAFUTA MAFUTA MENGI YA KUKAANGA kama chips, nyama choma nk, hatuli sana mboga mbichi mbichi za majani. Na zikipikwa zinachemshwa hadi zinageuka nyani.
Steamed Broccoli-F Macha
Mchanganyiko wa matango na brokoli, nilioutayarisha kwa “mvuke” – yaani kubandika sufuria yenye hizo mboga juu ya nyingine inayochemka chini yake. Upishi huu “barabara” hufanya mboga zisiunguzwe au kuiva sana- zinabakia imara.
Steaming pan-1
Steaming pans
WANGAPI TUNAKULA MATUNDA KWA WINGI AFRIKA?
Kiafya unatakiwa ule matunda aina tano kwa siku kupata faida zake zote mwilini.
Faida za matunda hazihesabaki. Na hayatakiwi yaliwe pamoja na chakula- bali kabla- AU KATI KATI YA MILO MIKUBWA. baadaye. Tabia yetu wengi kuchanganya matunda na milo mikubwa kama wali, ugali, chapati na kadhalika – hausaidii – ni afadhali hata usile kabisa.
Ndizi Mbivu
Ndizi mbivu toka visiwa vya Caribbean – huwa za aina moja tu. Hii ni kama ndizi tunayoita “mchare” kule Uchaggani.
Matunda humeng’enywa kwa vimeng’enyo tofauti na vyakula mama (wanga, protini, nk). Kati ya faida kuu za matunda ni:
1. Zuia maradhi , rutubisha na kinga mwili
2. Sukari , nguvu na mafuta asilia
3. Madini na Vitamin mbalimbali yanayosaidia kujenga, kukarabati na hata kuzuia bakteria na maadui wakubwa wakubwa wa miili yetu mathalan “free radicals”- tunaweza kulinganisha “free radicals” na majivu yanayobakia baada ya moto kuwaka. Hutolewa mwilini kama taka au kuingia mwilini kutokana na uchafu wa mazingira, mioshi ya sigara na magari, taka taka za mashine za kisasa – tena siku hizi wengi tunalala na simu za mkononi zikiwa zimewashwa, tunazibeba kwa wingi. Taka au majivu haya ndiyo kiini kikuu cha maradhi ya kisasa (nchi zilizoendelea) mathalan saratani.
Chenza
Ukipita maduka ya Uzunguni utakuta vyakula mbalimbali vinauzwa toka Afrika. Matunda haya yanayothaminiwa sana Majuu, huuzwa bei aghali sana.
Hapa London ambapo kila aina ya chakula ulimwenguni hupatikana bei za matunda ziko hivi, kiwastan:
1. Kichani kimoja cha ndizi kisukari (mara nyingi toka visiwa vya Ngazija au Mauritius) ni £2-£3. Kama shilingi 6-7,000. Ona chini ilivyo mbaya ukilinganisha na zinazopatikana Arusha, Mbeya au Kilimanjaro…
Ndizi Kisukari-pic by F Macha
2. Parachichi – hupimwa kufuatana na uzito. Kuna vijiparichichi vidogo vyeusi ambavyo vimejazana katika maduka makubwa makubwa (supamaketi) vijiparachichi koko- si vizuri hata kidogo- halafu aghali- mara nyingi si vitamu au vimeharibika ndani. Maparachichi makubwa makubwa toka Afrika nan chi za joto (tropics) hupatikana maduka ya pembe za chaki, kwa Wahindi au sokoni. Bei yake moja kiwastani ni £1.50- £2 kuendelea. Takriban 5,000.
Maparachichi Mawili-by F Macha
3. Maembe kiwastani ni kama maparachichi – ila miaka ya karibuni yameanza kupungua bei na hupatikana kirahisi (kufuatana na msimu). Maembe haya( kama mananasi ) hutoka Ivory Coast, Costa Rica na Brazil.
4. Papai-pia hupimwa kwa uzito. Makubwa hayapatikani kabisa katika supamaketi za Kizungu. Ukilitaka uende mitaa tunaoishi wageni, ya wafanyakazi , Wahindi na Waturuki. Haya yanatoka Brazil – bei yake ni £5 (Shilingi 12,000) kuendelea.
Tikiti Maji-1
5. Tikiti Maji- haya yako aina nne. Ya kijani nje, rangi ya chungwa ndani “Cantaloupe” yenye vitamin kibao huzwa wastani wa £1; ilhali manjano (toka Brazil) na kijani nje(toka Hispania ) wastani £2; aghali kuzidi yote ni tikiti maji lenyewe- kijani nje, jekundu ndani (“water-melon”);
£2.50 (Shs 6,000) kuendelea. Faida zake ki-afya hazisemeki.
6. Cherries na Strawberries. Matunda ya Kizungu. Kabla sijaja Majuu sikufaham Cherries, lakini Strawberry hupatikana maduka ya Kizungu Afrika.
Cherries
Mcheri…tunda lenye faida nyingi ikiwemo kusaidia maradhi ya Jongo.
Cherry ambalo hupendwa sana na ndege, lina faida nyingi sana miongoni kusaidia kupambana na maradhi yanayosakama damu au mzungunguko wa maji mwilini kama Jongo. Jongo ni ugonjwa unatokana na aidha kurithi, kunywa sana pombe, nyama nyekundu, mayai, kutofanya mazoezi. Hujionyesha kwa maumivu makali katika goti moja au kidole gumba cha mguu. Cherry safi sana. Vichache katika kasha huanzia £2 (Shilingi 5,000).
Strawberry- Stroberi kiwastani huwa aghali. Msimu yanapopungua bei ni wakati wa baridi (Desemba-Machi) yanaposhuka toka shilingi 7,000 hadi 5,000. Bei hizi hufuatana na wapi unaishi, maduka makubw ana madogo , nk
Kawaida sehemu tunazoishi Watanzania , kama mitaa ya Mashariki ya London kuna unafuu wa bei za vyakula na matunda shauri wakazi wengi hapa pia ni Wahindi wenye maduka ya bei nafuu kuliko ya yale makubwa makubwa ya Kizungu.
Apricot
7. Matunda yote yenye mbegu dani (Berries) kama Cranberries, Blue Berries, Blackberries- siku hizi hupatikana katika juisi zinazotengenezwa bila sukari nyingi. Nadhani tatizo kubwa la nchi Afrika ni kutengeneza juisi za matunda zilizojaa maji na sukari zaidi kuliko matunda. Huu ni udanganyifu na uroho wa wafanyabiashara wetu. Shirikisho la Ulaya limekuwa makini miaka ya karibuni kuzuia tabia hiyo Uzunguni na kuweka mikakati mikali.
Strawberries
Stroberi (Strawberry) – tunda linalopatikana zadi Uzunguni- ambalo lina Vitamin C kwa wingi.
Kifupi haya ndiyo matunda ya aghali rahisi hapa London.
Bei rahisi ni ndizi mbivu (toka visiwa vya Carribbean – na zingatia Matoke ya Uganda ni aghali sana- kichani kimoja kinaanzia shilingi elfu saba!), matufaha (matunda rasmi ya Kizungu), machungwa na machenza, Kiwi (yale matunda ya kijani toka New Zealand), zabibu, mapea (pears ), mapera, nk
Sasa tuongelee faida za matunda nliyoyachagua kwa leo yaani Mapapai na Maparachichi.
Ni muhimu kuzingatia kwamba matunda yanatakiwa kuliwa yakiwa katika kitengo kimoja- yaani chachu (“acid”), asidi au alkali (“alkaline”). Matunda hayo ya chachu ni maembe, mananasi, machungwa, zabibu, Kiwi, nk; ambapo alkali ni matikiti maji, ndizi mbivu, tufaha, mapea, Strawberry nk.
Acids-Mango Oranges Kiwi
Matunda chachu (“asidi”) yanatakiwa yaliwe pamoja…
Mapapai na Maparachichi yanaangukia katika mkondo wa “alkali” na moja ya matunda yaliyowekwa katika Vyakula Vyenye Nguvu kuliko vyote (Superfoods) . Matunda hayo ni Machungwa , Kiwi, Papai, Parachichi. Vyakula hivi via faida sana mwilini.
Alkalines-Apples Pears Ndizi-FMacha
Mfano wa matunda yenye “alkali” yanayotakiwa kuliwa pamoja.
Faida zake ni zifuatazo.
1. Kinga maradhi na kinga magonjwa (Anti-Oxidant) ambazo husaidia kukinga na kupambana na takataka zinazotolewa na mwili au zinazotoka katika mazingira machafu.
2. Vitamin C. Vitamin hii ni muhimu sana mwilini. Ukosefu wa Vitamin C husababisha uchovu, kukosa usingizi, uvivu, kutokuwa na hamu ya kula. Kwa siku mtu mzima unatakiwa upate gramu 40 za Vitamin C. Kwa wavuta sigara zidisha mara mbili. Ukila matunda yenye Vitamin C unapata kinga ya majeraha mwilini (vidonda pona haraka), huboresha wajihi, haiba na “nafsi” ya ngozi, mifupa, meno na mzunguko mzima wa damu mwilini- hivyo kusaidia usingizi ( na kwa watoto kusaidia kukua vizuri).
Papai-1-pic by F Macha
3. Papai lina “papain” inayosaidia kuukinga mwili na kulainisha tumbo- ndiyo maana kama umevimbiwa au huendi haja kubwa sawasawa (“constipation”) ukila papai husaidia sana.
4. Mapapai na Maparachichi yana “Beta Carotene”(itokanayo na Vitamin A) inayopatikana pia katika nyanya, karote, maembe, mchicha (ambao haukupikwa hadi ukanyong’onyea), mbegu mbegu (mbichi si za kukaanga au kuwekwa chumvi- hadi zikakongoroka) kama hizi pichani chini karanga, mlozi, korosho, nk.
Mseto wa Mbegu Mbichi
Faida zake ni pamoja na kusaidia mizunguko ya umajimaji na damu mwilini, ngozi na nywele (safi sana kwa kina dada wanaojipenda), kupunguza mafuta katika damu (cholestoral) na “presha” – mambo yanayoua sana watu weusi duniani leo. Ukiwa upungufu wa “Beta Karotene” macho hayaoni vizuri, unaugua upesi upesi hasa maradhi ya mapafu (mafua, kikohozi,nk). Kwa wanawake waja wazito ni rahisi kupoteza watoto au kuzaa watoto ambao hawako sawasawa.
5. Maparachichi yanayo mafuta asilia. Mafuta haya ni mazuri SANA kuliko yale tunayoyapata katika nyama au vitu vilivyokaangwa, maana yanausaidia na haya haribu mwili. Makisio yake ni kalori 400 kwa parachichi moja. Hiyo ni nguvu kubwa sana. Ndiyo maana Parachichi (na Papai) huhesabiwa kama mfalme wa matunda.
Papai na Parachichi -nje
Lazima izingatiwe kuwa chakula, mmea au tunda lolote lenye rangi nzito iliyokolea kama parachichi huwa na faida MARIDHAWA mwilini.
Hivyo, kuanzia leo kama hukua ukithamini matunda haya mawili- kayatafute. Kuna watu wazima wanaosema eti matunda ni chakula cha watoto. Wanakosea. Mtu mzima anahitaji kuendelea kuukarabati mwili wake. Kwetu Afrika ni ya bei nafuu- wapo wengi wanaofika Ulaya na Marekani wanashindwa kuyala shauri bei yake si mchezo. Halafu wala si matamu kama ya nyumbani Afrika…

Comments

Popular posts from this blog

KUTOKWA NA UCHAFU UKENI, CHANZO NA TIBA YAKE

Uke wa mwanamke hufanya kazi ya kutoa njia kati ya sehemu ya nje ya mwili na viungo vya uzazi vya ndani vya mwanamke. Hali ya kawaida ya majimaji yaliyomo katika uke wa mwanamke huwa ni ya tindikali ili kuzuia maambukizi ya vijidudu wa kuleta maradhi. Hali hii ya utindikali huletwa na bacteria waishio katika uke wa mwanamke. Bacteria hawa ni wa kawaida na hawana madhara kwa mwili. Uke ulio katika hali nzuri hutoa majimaji haya ili kujisafisha. Majimaji haya yanayotengenezwa katika uke na kwenye eno la cervix hufanya kazi ya kuondoa seli zilizokufa na bacteria waharibifu nje ya mwili na huu ndio uchafu wa kawaida ambao mwanamke hutoa ukeni. Kutoa uchafu huu sehemu za siri ni njia ya kuusafisha uke na kuzuia maambukizi ya magonjwa. Kitu cho chote ambacho kitaharibu uwiano wa utengeneaji wa majimaji haya ndani ya uke kinaweza kujenga mazingira ya maambukizi katika uke. Uchafu Wa Sehemu Za Siri  Wa Kawaida Wanawake wote hutoa uchafu sehemu za siri. Kiwango cha uchafu unaotoka, ra

JINSI YA KUONGEZA UFANISI WA VICHOCHEO VYA KIUME (TESTOSTERONE) NA KUKINGA DHIDI YA MATATIZO YATOKANAYO NA KUKUA KWA TEZI DUME KWA KUTUMIA VYAKULA HIVI VI 5

Maelezo ya utangulizi. Kichocheo cha testosterone, japo huusishwa zaidi na upande wa mwananume ni muhimu kwa afya ya pande zote mbili yaani mwanamke na mwanamme pia.kadiri umri unavoenda mbele basi kiwango cha uzalishaji wa kichocheo cha testerone kupungua, kupungua kwa kichocheo hiki kunaambatana na ukuaji wa tezi dume (prostate gland),kupotea kwa nywele na pia saratani mfano saratani ya tezi dume. .KAZI KUBWA YA KICHOCHEO HIKI NI KUONGEZA MSUKUMO NA HAMU YA TENDO LA NDOA , KUIMARISHA MISULI NA MIFUPA MWILINI. NINI KINAHITAJIKA ILI KUZALISHA KICHOCHEO CHA TESTOSTERONE? Ili kuhakikisha uzalishaji wa kichocheo cha kiume unafanyika, mwili unahitaji virutubisho au viini lishe mbalimbali, baadhi ya viini lishe hivyo ni madini ya ZINC na vitamin D3,  vitamini D inaweza kuzalishwa na mwili pale ngozi yako inapokutana na mwanga wa jua, hapa nazungumzia mwanga wa asubuhi wakati jua ndo linachomoza na pia lile jua la jion karibia na kuzama, hivyo utakubaliana na mimi kuwa wengi wet

MADHARA YA PUNYETO NA TIBA YAKE

MAELEZO  YA AWALI KUHUSU TATIZO LA UPIGAJI PUNYETO Watu wengi sana wanataka kufahamu jinsi gani wafanye ili kuachana na kitendo cha upigaji punyeto. Punyeto ni tendo la mtu la kuamsha hisia za mapenzi au msisimko ambao unampelekea mtu huyu kufikia kilele cha kujimalizia tamaa zake! Bila kufanya tendo halisi, hutumia fikra zake katika picha za zinazoitwa za ngono au picha zozote zinazoweza kulifanikisha tendo hilo, movie n.k. Kilele cha yote anafikia mahali anajimalzia tamaa zake mwenyewe!. Nimekuwa nikiona baadhi ya watu wanaosema wameelimika wakipingana wao kwa wao katika suala zima la kupiga punyeto! Wako wanaotetea kutokana na elimu yao na wanasema kwa ujasiri mkubwa kwamba "kupiga punyeto ni sehemu ya maisha ya mwanadamu" Ina maana katika maisha ya mwanadamu upigaji punyeto inaelezwa ni kama tendo la lazima mpaka inafikia mahali wanasema ni sehemu ya maisha (Maisha) ya mwanadamu. Nimekuwa nikipata kesi nyingi sana juu ya madhara yatokanayo na punyeto. Aslimia 60